Raia thelathini wauawa katika kijiji kimoja nchini Nigeria
Takriban raia 30 waliuawa siku ya Jumamosi katika shambulio dhidi ya kijiji kimoja lililofanywa na watu wanaoshukiwa kuwa wafugaji wa kabila la Fulani katika jimbo la Nigeria ambapo ghasia kati ya wafugaji wanaopigania maji na nyasi ni za mara kwa mara, afisa wa eneo hilo ameliambia shirika la habari la AFP siku ya Jumanne.
Imechapishwa:
Washambuliaji walivamia kijiji cha Runji kaskazini magharibi mwa Nigeria saa moja usiku. Waliwafyatulia risasi wakazi na kuchoma nyumba huku watu wakijaribu kukimbia, amesema Francis Sani, rais wa utawala wa eneo la Zangon Kataf. "Tulizika watu 33 waliouawa katika shambulio la Jumapili, wakiwemo wanawake na watoto," ameongeza wakati wa mahojiano ya simu.
Washambuliaji hao ambao bila shaka ni wafugaji wa kabila la Fulani pia walichoma moto nyumba zaidi ya 40 katika kijiji hicho kabla ya kukabiliana na askari na wanamgambo waliotahadharishwa," afisa wa eneo hilo amesema. Watu sita pia walijeruhiwa katika shambulio hilo siku tatu baada ya vifo vya raia wanane katika shambulio kama hilo katika kijiji jirani, Francis Sani amesema.
Katika taarifa yake siku ya Jumapili, Samuel Aruwan, kamishna wa masuala ya usalama wa ndani katika jimbo la Kaduna, ambalo kusini mwa nchi hiyo kuna Wakristo wengi, alithibitisha shambulio hilo kuwa "halikubaliki". "Watu kadhaa walipoteza maisha," amesema bila kutoa maelezo.
Ukosefu wa usalama nchini Nigeria utakuwa mojawapo ya changamoto kuu kwa Rais mteule Bola Tinubu, ambaye alishinda uchaguzi wa rais mwezi Februari uliokumbwa na matatizo ya kiufundi na shutuma za upinzani kwa udanganyifu.