Kesi ya Kabuga Felicien yaanza kusikilizwa ICC
Kesi dhidi ya Felicien Kabuga, raia wa Rwanda anayedaiwa kufadhili kwa kutoa fedha mauaji ya kimbari mwaka 1994, yaliyosababisha vifo vya watu zaidi ya 800,000, wengi wao wakiwa ni Watutsi, inaanza kusikilizwa hivi leo, kwenye Mahakama maalum ya Umoja wa Mataifa, jijini Hague nchini Uholanzi.
Imechapishwa:
Kabuga, ambaye kwa sasa ana umri wa miaka 87, anadaiwa kutumia chombo cha habari na kuwahimiza Wahutu kuwauwa Watutsi, lakini pia kutoa fedha zilizonunua mapanga kwa ajili ya kutekeleza mauaji hayo.
Baada ya kutafutwa kwa muda mrefu, Kabuga alikamatwa nchini Ufaransa mwaka 2020 na kusafirishwa jijini Hague kufunguliwa mashataka katika Mahakama hiyo maalum ya Umoja wa Mataifa.
Viongozi wa mashtaka siku ya Alhamisi na Ijumaa, watafafanua mashtaka dhidi ya Kabuga na baadaye kuwasilisha ushahidi kuanzia tarehe tano Oktoba.
Ripoti zinasema kuwa, mashahidi zaidia ya 50 watatoa ushahidi dhidi ya Kabuga katika kesi hii.
Tayari mawakili wa Kabuga mwaka 2020 waliiambia Mahakama kuwa, mteja wao anapinga mashtaka dhidi yake, na jitihada za kusitisha kesi hiyo kwa sababu ya hali mbaya ya kiafya ya Kabuga, haijafua dafu.
Haijafahamika iwapo, Kabuga mwenyewe atakuwa Mahakamani, lakini Majaji waliamua kuwa anaweza kufika Mahakamani kupitia mkanda wa vídeo kwa sababu ya hali yake ya kiafya.