Serikali ya Kenya yatangaza Ijumaa siku ya mapumziko ya kuwakumbuka wahanga wa mafuriko
Serikali ya Kenya imetangaza siku ya Ijumaa kuwa siku ya mapumziko kuwakumbuka watu waliopoteza maisha kutokana na mafuriko na kupanda miti kupambana na mabadiliko ya tabia nchi.
Imechapishwa:
Akizungumza kwenye kikao kaunti ta Kajiado rais amesema siku hiyo ambayo itakuwa Mei 10 aidha itatumika kukumbuka maisha ya Wakenya walioathirika na walioaga dunia kutokana na mafuriko katika maeneo mbalimbali nchini.
Kadhalika rais Ruto ameongeza kuwa siku hiyo pia imetengwa kwa ajili ya zoezi la upanzi wa miti ikiwa ni njia moja wapo ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.
Mapema leo Msemaji wa Serikali Isaac Mwaura aliandika kwenye akaunti ya X kuwa; “Notisi ya Gazeti rasmi la serikali itatolewa kwa athari hii. Waziri wa Mazingira, Misitu na Mabadiliko ya Tabianchi, Soipan Tuya atahutubia waandishi wahabari leo kutoa maelekezo zaidi.”
Katika taarifa ya hivi punde ya serikali kuhusu athari ya mafuriko kote nchini msemaji wa serikali amesema kwamba kufikia sasa takriban watu 75 kote nchini hawajulikani waliko, huku watu 238 wakiwa wameaga dunia kutokana na mafuriko yanayoshuhudiwa nchini