Félicien Kabuga hajaripoti mahakamani katika siku ya kwanza ya kesi yake
Miaka 28 baada ya mauaji ya kimbari nchini Rwanda, kesi ya anayedaiwa kuwa "mfadhili", Félicien Kabuga, imeanza kusikilizwa Alhamisi hii, Septemba 29 huko Hague, Uholanzi. Mfanyabiashara huyo wa zamani, ambaye sasa ana umri wa miaka 87, anatuhumiwa kuwa na jukumu "muhimu" katika mauaji ambayo yaliua zaidi ya watu 800,000 kati ya mwezi Aprili na Julai 1994, hasa miongoni mwa Watutsi walio wachache.
Imechapishwa:
Hali yake ya afya "ni nzuri" lakini Félicien Kabuga, ambaye bado amedhoofika, amependelea kutohudhuria kesi hiyo, ama ana kwa ana au kwa njia ya video, amebaini mmoja wa mawakili wa upande wa mashtaka. Kesi hii inasubiriwa kwa hamu, na upande wa mashtaka umeeleza kuwa inakuja kwa kuchelewa sana, miaka 28 baada ya tukio la mauaji. Ananuia kumwajibisha Félicien Kabuga kwa uhalifu wake. Huenda hakulazimika "kushika bunduki au panga," lakini alikuwa kitovu cha ufadhili wa propaganda za mauaji ya halaiki, upande w mashtaka umesema.
Zaidi ya mashahidi 50 wanatarajiwa kusikilizwa
Akichukuliwa wakati huo kuwa mmoja wa watu tajiri zaidi nchini Rwanda, alitumia bahati yake kuanzisha na kusimamia kituo maarufu cha Radio na televisheni RTLM, "Radio-télévision libre des mille collines", ambacho, katika kilele cha mauaji ya halaiki, kilieneza hotuba za chuki dhidi ya Watutsi, masaa 24 kwa siku.
Sehemu ya moja ya matangazo ilionyeshwa na kusikilizwa wakati wa kesi. Kunasikika waandishi wa habari wakilinganisha Watutsi na mende ambao walipaswa kuangamizwa.
Upande wa mashtaka pia uliwataja mashahidi wanaothibitisha jinsi Kabuga alivyofadhili na kutoa mafunzo kwa wanamgambo wa Kihutu wa Interahamwe, ambao ndio watuhumiwa wakuu wa mauaji hayo.
Kuanzia Jumatano ijayo, Oktoba 5, upande wa mashtaka utawasilisha ushahidi huo. Zaidi ya mashahidi 50 wanatarajiwa kusikilizwa. Kesi itaendelea Ijumaa asubuhi Septemba 30.