Mjadala mkali waendelea kuhusu wakimbizi na wahamiaji, viongozi wa dunia watofautiana
Baadhi ya mashirika ya haki za binadamu duniani yamepongeza hatua iliyofikiwa na viongozi wa dunia, ambao mwanzoni mwa juma hili, waliidhinisha azimio lililolenga kuratibu misaada zaidi ya kibinadamu kwa wakikmbizi ambao wamesababisha mgawanyiko mkubwa kutoka barani Afrika hadi Ulaya.
Imechapishwa:
Jumatatu ya wiki hii, wakuu wa dunia walipitisha kwa kauli moja azimio maalumu litakalo hakikisha kuwa nchi zilizoendelea zinatoa misaada na kufanikisha kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa fedha zitakazowezesha kukabiliana na wimbi la wakimbizi.
Suala la nini kifanyike kuhusu watu zaidi ya milioni 65 duniani ambao hawana mahali pakuishi, ni suala ambalo limekuwa ajenda kuu ya mkutano wa 71 wa baraza la umoja wa Mataifa uliong’oa nanga jijini New York, Marekani.
Viongozi kutoka mataifa 193 wanachama wa umoja wa Mataifa wanakutaka kwenye mkutano huu wa kihistoria ambao unajadili namna bora zaidi ya kukabiliana na wimbi la wahamiaji na wakimbizi.
Wakizungumza kwenye kando kwenye mkutano maalumu wa kimataifa kuhusu wakimbizi na wahamiaji, baadhi ya wanaharakati wa haki za binadamu wameoneshwa kutoridhishwa na maazimio haya licha ya kuyaunga mkono, wakisema kuwa pamoja na kukubaliwa, linakosa mamlaka kisheria kama inavyohitajika katika mikataba ya umoja wa Mataifa.
Hata hivyo katibu mkuu wa umoja wa Mataifa Ban Ki Moon ambaye wakati mmoja yeyey mwenyewe akiwa mkimbizi kutoka Korea, amepongeza akisema kupitishwa kwa azimio hilo ni hatua ya kihistoria.
Duniani kote, kwa sasa inakadiriwa kuna wakimbizi milioni 21 na laki 3, waomba hifadhi milioni 3 na laki 2 na wahamiaji milioni 40 na laki 8, na hii ni kwa mujibu wa shirika la umoja wa Mataifa linalohusika na wakimbizi.
Rais wa Marekani, Barack Obama, September 20 mwaka huu ameongoza kikao maalumu cha wakuu wengine wa nchi kuzungumzia suala la wakimbizi na wahamiaji, ambapo mambo kadhaa yamekubaliwa ikiwemo namna ya kuongeza upatikanaji wa fedha, kukubali kupokea wakimbizi zaidi kwa baadhi ya nchi pamoja na kutoa elimu na uelewa kwa wakimbizi na wahamiaji.
Azimio hili linataka kuwepo kwa usawa na kuheshimiwa kwa haki za binadamu hasa kwa wakimbizi na wahamiaji kupewa elimu sawa na wengine na hasa kwa watoto ambao wanatengeneza nusu ya idadi ya wakimbizi wote duniani.