Kenya: Maandamano ya upinzani kufanyika mara tatu kwa wiki
Nairobi – Upinzani nchini, umetangaza kufanyika kwa maandamano dhidi ya serikali kwa siku tatu mfululizo wiki ijayo kuanzia Jumatano hadi Ijumaa.
Imechapishwa:
Katika taarifa iliyotolewa siku ya Ijumaa, muungano huo ulisema kutokana na matakwa ya raia, umelazimika kuangazia upya mpango wake wa awali wa kufanya maandamano siku ya Jumatano pekee.
Haya yanajiri licha ya onyo kali la serikali ambayo imeapa kutoruhusu maandamano hayo ambayo yamesababisha vifo vya watu kadhaa, wengine wengi wakiripotiwa kujeruhiwa na mali ya thamani isiyojulikana kuharibiwa.
Siku ya Alhamisi, Rais William Ruto aliwakashifu mtangulizi wake Uhuru Kenyatta na kinara wa upinzani Raila Odinga kuhusu kile alichokitaja kuwa kuandaa machafuko nchini kwa kisingizio cha maandamano ya amani dhidi ya serikali.
Rais Ruto alimshutumu Odinga kwa kujaribu kuhujumu serikali zote tatu zilizopita kwa akiwa na nia ya kuingia kwenye serikali kwa kupitia mlango wa nyuma.
Waziri wa usalama wa ndani nchini humo Kithure Kindiki naye pia alilaani vitendo vya ghasia, uporaji na uharibifu wa mali vilivyoshuhudiwa katika sehemu mbalimbali za nchi siku ya Jumatano wakati wa maandamano ya kupinga kupanda kwa gharama ya maisha.
Aidha waziri huyo aliapa kuhakikisha kwamba watu wote walioshiriki maandamano, moja kwa moja na kwa njia isiyo ya moja kwa moja, watawajibishwa kwa mujibu wa sheria.