Mazungumzo kati ya pande mbili hasimu nchini Libya kuanza tena nchini Morocco
Morocco inajiandaa kupokea wajumbe kutoka pande mbili hasimu nchini Libya wiki ijayo. Bunge la Libya lenye makao yake Tobruk, mashariki mwa nchi, na kwa upande mwingine, Baraza Kuu la Kitaifa, lenye makao yake mjini Tripoli.
Imechapishwa:
Baraza Kuu la Kitaifa nchini Libya linachukuliwa na utawala wa Tripoli kuwa ni Baraza la Seneti chini ya makubaliano ya Skhirat yaliyofikiwa mwezi Desemba 2015, lakini taasisi hiyo haitambuliwi na Baraza la wawakilishi nchini humo.
Mkutano huu ni wa kiishara, kwa lengo la kujaribu kuimarisha hatua ya usitishwaji mapigano iliyotangazwa wiki iliyopita na kuzindua tena mchakato wa kisiasa.
Kamati mbili za mazungumzo, kila moja ikiundwa na watu 7, ziliundwa kwa minajili ya mazungumzo na kujaribu kusonga mbele kuhusu tofauti kati ya pande hizo mbili.
Kwa pande zote mbili, wanasema mikutano hii "itawezesha kufufua uhusiano uliovunjika" kwa zaidi ya miezi 15, kwa sababu ya mashambulizi yaliyoongozwa na Marshal Khalifa Haftar ili kudhibiti mji mkuu wa Tripoli.
Kulingana na vyanzo kutoka kambi zote mbili ambavyohavikutaja majina, majadiliano haya, ambayo yatadumu siku kadhaa, yanalenga "kuondoa matatizo na kukubaliana juu ya masuala kadhaa ya mpango wa Aguila Saleh", Spika wa Bunge la Mashariki. Mikutano hiyo pia inalenga kukubaliana juu ya "kugawana madaraka na mapato ya mafuta".