Cameroon kumjengea nyumba ya kifahari Jaji aliyemtangaza rais Biya mshindi
Serikali ya Cameroon imetangaza zabuni ya kumjegea nyumba ya kifahari rais wa Mahakama ya Katiba, aliyemtangaza rais Paul Biya mshindi wa Uchaguzi wa urais, kuendelea kuongoza nchi hiyo kwa muhula wa saba.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Hatua hii imezua maswali mengi nchini Cameroon, wengi wakiona kuwa ni kama zawadi kwa rais huyo wa Mahakama kwa kumtangaza Biya mshindi wa Uchaguzi wa urais uliofanyika Oktoba 7.
Ujenzi wa nyumba hiyo inatarajiwa kukamilika baada ya miezi minane na kuigharimu serikali Dola 473,000.
Mahakama wiki iliyopita, ilitupilia mbali kesi 18 za kupinga ushindi wa rais Biya amabye ameongoza nchi hiyo kwa miaka 36.
Biya anaugana na rais wa Equitorial Guinea Teodoro Obiang Nguema kama viongozi waliokaa madarakani kwa muda mrefu.
Viongozi wa upinzani wamekataa kutambua ushindi wake, wakati huu hali ya wasiwasi ikiendelea kushuhudiwa maeneo yanayozungumza lugha ya Kiingereza.