Upinzani nchini Kenya waonya dhidi ya ubadilishaji wa sheria ya kuhesabu kura
Muungano wa upinzani nchini Kenya NASA, unasisitiza kuwa uchaguzi nchini humo hautafanyika mwezi Agosti mwaka huu ikiwa Mahakama ya rufaa itabadilisha sheria ya Uchaguzi.
Imechapishwa:
Tume ya Uchaguzi ilikwenda katika Mahakama hiyo kupinga agizo la Mahakama kuu kuwa matokeo ya mwisho ya urais yatakayotangazwa katika maeneo bunge, ndio yatakayokuwa ya mwisho.
Hata hivyo, Tume inaonya kuwa huenda maafisa wake wakafanya makosa katika mahesabu yao na hivyo wanataka kupitia matokeo hayo kabla ya kutoa matangazo ya mwisho.
Mgombea urais kupitia muungano wa upinzani Raila Odinga amesema serikali imetumia Tume ya Uchaguzi kwenda Mahakamani kushawishi kubadilishwa kwa sheria hiyo ili kuiba kura.
“Hatutakubali Tume ya Uchaguzi kuingilia uamuzi wa Mahakama kuhusu ujumuishwaji wa matokeo,”
“ Ikiwa watajaribu kufanya hivyo basi wafahamu kuwa hakuna uchaguzi utakaofanyika,” alisema Odinga wakati akiwahotubia wafuasi wake mjini Nakuru.
Hata hivyo, serikali imeshtumu matamshi hayo na kusema yanalenga kuingilia shughuli za Mahakama.
Uchaguzi umepangwa kufanyika tarehe 8 mwezi Agosti huku ushindani mkali ukitarajiwa kuwa kati ya Raila Odinga na rais Uhuru Kenyatta.
Kampeni rasmi zinatarajiwa kuanza tarehe 28 mwezi huu na zitadumu kwa muda wa miezi mitatu.