Maandamano ya kupinga ukatili dhidi ya wanawake yafanyika jijini Nairobi
Nairobi – Mamia ya watu wameandamana jijini Nairobi kukashifu visa vya ukatili dhidi ya wanawake ambavyo vimekuwa vikiripotiwa katika baadhi ya maeneo nchini Kenya.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Wanawake kadhaa wameripotiwa kuuawa mwezi huu wa Januari,matukio ambayo yamelaaniwa na mashirika ya kutetea haki za binadamu kwenye taifa hilo.
Karibia wanawake 16 wamethibitishwa kuuawa nchini Kenya mwaka huu peke kwa mujibu wa ripoti za vyombo vya habari vya ndani.
Tukio la hivi punde ni la mwanamke mwenye umri wa miaka 26 aliyeuawa tarehe nne ya mwezi huu wa Januari katika chumba cha kupanga nje kidogo na mji wa Nairobi.
Takriban wiki mbili baadaye, mwanamke mwenye umri wa miaka 20 alinyongwa, kukatwa vipande vipande na mabaki yake kuingizwa kwenye mfuko wa plastiki.
Wanaume wawili wanazuiliwa na polisi kuhusiana na kesi hiyo lakini bado hawajafunguliwa mashtaka.
Zaidi ya asilimia 30 ya wanawake nchini Kenya wanakabiliwa na ukatili , asilimia 13 wanapitia aina tofauti ya ukatili wa kingono, kulingana na ripoti ya serikali iliyotolewa mwaka jana.
Crowd chants 'where were you' and 'go back home' at Nairobi Women Rep Esther Passaris at Jevanjee Gardens #EndFemicideKE #TotalShutDownKE pic.twitter.com/G8ADtx42Wc
— Nation Africa (@NationAfrica) January 27, 2024
Kulikuwa na angalau visa 152 vya mauaji ya wanawake nchini Kenya mwaka jana, kulingana na shirika la kiraia la Femicide Count ambalo huweka hesabu ya matukio yaliyoripotiwa pekee.
Mnamo 2022, wanawake na wasichana wapatao 725 waliuawa katika nchi hiyo ya Afrika Mashariki, kulingana na ripoti kutoka mashirika ya UN.