Kenya: Ziara ya mfalme wa Uingereza inakabiliwa na shinikizo
Mfalme wa Uingereza Charles wa Tatu anayetazamiwa kuwasili nchini Kenya kwa ziara rasmi ya siku nne ,anakabiliwa na shinikizo kutoka mashirika ya kiraia na wanaharakati wa haki za binadaam wanaosisitiza sharti aombe radhi kwa mateso ambayo Uingereza iliwapa wakenya wakati wa ukoloni.
Imechapishwa:
Mashirika haya siku ya jumapili yakiongozwa na shirika la Kenya Human Rights Commission,yalitoa makataa kuwa msamaha huo sharti uwe wa dhati na utolewe hadharani.
Hii inakuja wakati mashirika mengine haswa yanayowakilisha waathiriwa wa mateso hayo ,yakiapa kufanya maandamano licha ya polisi na pia ubalozi wa Uingereza Kenya kupiga marufuku maandamano yoyote wakati wa ziara ya mfalme Charles na malkia Camilla.
Kuna zaidi ya watu elfu 10 waliowauwa na mamlaka za Uingereza kabla Kenya kupata uhuru wengine elfu moja wakinyongwa baada ya kufungwa jela.
Miaka kumi iliyopita Uingereza ilikiri rasmi kuwa watawala Wake walihusika na vitendo vya ukatili na mateso hayo.
Baadhi ya jamii zilizoathirika nchini Kenya ni Nandi ,Kipsigis na Pokot na zimekuwa zikipigania kulipwa fidia,kufuatia ukatili huo wa kihistoria .