Burundi: Gavana wa zamani wa benki kuu Murengerantwari amekamatwa na polisi
Gavana wa benki kuu ya Burundi aliyeondolewa afisini hivi majuzi amekamatwa kwa tuhuma za ufisadi.
Imechapishwa:
Dieudonné Murengerantwari anatuhumiwa na wizara ya sheria kwa madai ya kuhujumu utendakazi mzuri wa uchumi wa taifa, ufisadi, ufujaji wa pesa na ufujaji wa mali ya umma.
Licha ya tuhuma hizo, kiongozi huyo wa zamani hajajibu madai hayo.
Siku ya Jumapili, Rais wa Burundi Évariste Ndayishimiye alimfuta kazi Murengerantwari na nafasi yake kuchukuliwa na Édouard Normand Bigendako.
Murengerantwari alikuwa ameteuliwa kuongoza benki kuu ya Burundi kwa miaka mitano kuanzia Agosti mwaka jana.
Kwa mujibu wa mwanasheria mkuu wa Burundi Leonard Manirakiza, uchunguzi zaidi kuhusu madai hayo ya ufisadi dhidi ya kiongozi huyo unaendelea.
Aidha taarifa ya mwanasheria huyo mkuu wa Burundi inasema gavana huyo wa zamani wa benki kuu kwa sasa anashughulikiwa kwa mujibu wa sheria wakati akiendelea kuzuiliwa.