DRC: Makabiliano yaripotiwa kati ya M23 na makundi hasimu mjini Masisi
Nairobi – Mapigano zaidi yameripotiwa mashariki mwa nchi ya DRC kwenye mji wa Masisi, kati ya waasi wa M23 na makundi hasimu yenye silaha.
Imechapishwa:
Cheza - 00:47
Kwa mujibu wa vyanzo kutoka kwenye maeneo hayo, mapigano yalianza tena hapo jana katika maeneo ya Nturo-Kilolirwe, Ruvunda na Bashali Kahembe.
Mashirika kadhaa ya kiraia yamethibitisha kutokea kwa makabiliano hayo kwenye njia ya Kibarizo, mjini Bashali Mokoto.
Haya yanajiri baada ya Jumatano ya wiki hii kuripotiwa mapigano mengine katika miji ya Kibarizo, Kirumbu na Busumba, mashuhuda wakidai kundi la M23 limeongeza wapiganaji wake kwenye maeneo hayo.
Hata hivyo hadi sasa imekuwa si rahisi kuthibitisha upande gani unaongoza eneo gani, ingawa baadhi ya vyanzo vinasema maeneo kadhaa yanakaliwa na wapiganaji wa pande zote mbili.
Mapigano haya yanajiri wakati huu kukiwa na hofu ya machafuko zaidi mashariki mwa nchi hiyo, ambayo yanaweza kutatiza shughuli za kuelekea uchaguzi wa Desemba 20.