Kenya: Maandamano ya siku tatu ya upinzani kuaanza wiki hii
Wakati huu raia wa Kenya wakijiandaa kwa maandamano mengine ya upinzani yanayotarajiwa kufanyika kwa siku tatu mfululizo kuanzia Jumatano ya wiki hii, wanasiasa wanaokinzana wameendelea kuvutana hali inayotishia kutokea vurugu wakati wa maandamano hayo.
Imechapishwa:
Akizungumza katika moja ya mikutano aliyoifanya mwishoni mwa juma lililopita, waziri wa mambo ya ndani Kithure Kindiki, aliapa idara za usalama kuwashughulikia kikamiilifu aliowaita wahalifu wanaojificha nyuma ya kivuli cha katiba.
Juma lililopita rais William Ruto, alimuonya kinara wa upinzani Raila Odinga, akisema maandamano ya wiki hii hayatakubalika na wahusika wanatakabiliwa na mkono wa sheria, hii ni baada ya yale ya wiki iliyopita kushuhudia vurugu ambapo watu 13 walipoteeza maisha.
‘‘Ndugu zangu wa upinzani tafadhali tufanye siasa kwa amani tuuze sera zetu, sijasema mkubaliane na serikali na wale wanaounga mkono serikali musilazimishe watu wakubaliane na sera za serikali wako na uhuru wa kuwa na maoni tofauti.’’ alisema waziri Kithure Kindiki.
Kithure Kindiki, Waziri wa usalama nchini kenya
Vyama vya walimu nchini Kenya, vimetoa wito kwa rais William Ruto na kinara wa upinzani, Raila Odinga kufanya mazungumzo na kusitisha maandamano ambayo yamepangwa kufanyika siku tatu kila wiki, vyama hivyo vikisema maandamano hayo yamesababisha kuathirika masomo.
Kando na vyama vya waalimu, viongozi wa kidini pia wamekuwa wakitoa wito kwa pande hizo mbili kufanya mazungumzo na kumaliza mzozo uliopo kwa sasa unaotishia kulitumbukiza taifa hilo la Afrika Mashariki katika mzozo.
Upinzani umesisitiza kwamba maandamano yake yataendelea kama ilivyopangwa licha ya onyo kutoka kutoka kwa serikali kuwa haitaruhusu kufanyika kwa maandamano mengine nchini humo.
Odinga na mrengo wake wanasema maandamano hayo yanalenga kuishinikiza serikali ya rais Ruto kuhakikisha kwamba inashugulikia suala la kupanda kwa gharama ya maisha.