Kenya: UN yawaonya polisi kutowakabili waandamanaji kwa nguvu kupita kiasi
Nairobi – Ofisi ya haki za kibinadamu katika umoja wa mataifa imeeleza kusikitishwa na ghasia zinazoendelea nchini Kenya pamoja na madai ya matumizi ya nguvu yasiyo ya lazima ikiwa ni pamoja na matumizi ya silaha za moto, na polisi wakati wa maandamano.
Imechapishwa:
Ripoti zinasema hadi sasa watu 23 wameuawa na makumi ya wengine kujeruhiwa katika maandamano hayo ya wiki iliyopita.
UN inasema inatoa wito kwa uchunguzi wa haraka, wa kina, huru na wa uwazi kuhusu vifo na majeruhi. Waliohusika lazima wawajibishwe. Hatua madhubuti za kuzuia vifo na majeraha zaidi lazima zichukuliwe.
Kwa kuzingatia wito wa maandamano zaidi wiki ijayo, umoja wa mataifa umetoa wito kwa mamlaka kuhakikisha haki ya kukusanyika kwa amani kama inavyothibitishwa na Katiba ya Kenya na sheria za kimataifa za haki za binadamu.
Aidha UN imetaka kuwepo kwa utulivu na kuhimiza mazungumzo ya wazi ili kushughulikia malalamishi ya kijamii, kiuchumi na kisiasa, kwa lengo la kubainisha suluhisho la kudumu kwa maslahi ya Wakenya wote.