Kenya : Rais Ruto awaonya wapinzani dhidi ya maandamano
Nairobi – Muungano wa upinzani nchini Kenya, hivi leo unatarajiwa kufanya maandamano zaidi kupinga kile unasema kupanda kwa gharama za maisha pamoja na kuongezwa kwa kodi zinazoumiza wananchi, maandamano ambayo hata hivyo yamezuiwa na polisi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Hadi tukichapisha taarifa hii, maeneo mbalimbali jijini Nairobi yalionekana kuwa tulivu licha ya uwepo mkubwa wa maofisa wa polisi wa kupambana na ghasia.
Tofauti na maandamano ya awali, upinzani umeonekana kubali mkondo ambapo kwa sasa yanafanyika katika maeneo ya mikoa suala ambalo mrengo huo unasema linalenga kuwahusisha raia kutoka maeneo tofauti.
Hatua ya polisi ilipazwa sauti na rais William Ruto, ambaye amesisitiza kutokubali watu wachache waharibu amani ya nchi.
‘‘Wale ambao muko na maamuzi mahali ambapo mupo mujuwe yakwamba hamuwezi kuharibu ajira ya wakenya milioni moja.’’ alisema rais Ruto.
Rais wa Kenya, William Ruto
Kwa upande wake kinara wa upinzani Raila Odinga, amesisitiza kuendelea na maandamano hadi pale haki itakapopatikana akiwataka wakenya kujitokeza kwa wingi wakati wa maandamano hayo.
‘‘Nataka wakenya wote kila mahali wafuasi wa Azimio na hata wale wa Kenya Kwanza wajitokeze ili kuonyesha kuwa punda amechoka.’’ alisema Raila Odinga.
Raila Odinga, kinara wa upinzani nchini Kenya
Ikiwa yatafanyika yatakuwa ni maandamano ya pili katika muda wa wiki moja baada ya yale ya Ijumaa ya wiki iliyopita ambapo watu 6 walipoteza maisha.