Kenya: Raila asisitiza kuwepo maandamano ya Jumatano
NAIROBI – Kiongozi wa muungano wa Azimio la Umoja-One Kenya, Raila Odinga, amezindua rasmi mchakato wa kukusanya sahihi milioni 15 kwa ajili ya wakenya kuonyesha kutoridhishwa kwao na jinsi serikali ya Kenya Kwanza inaendesha shughuli zake.
Imechapishwa:
Cheza - 00:30
Raila amesema mchakato huu unafanyika kupitia wavuti wa www.tumechoka.com ambao tayari umeanza kufanya kazi, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya upinzani, ili kumlazimisha rais William Ruto na utawala wake kuheshimu na kuwasikiliza raia.
Wabunge na rais wameungana pamoja dhidi ya raia, na raia wameachwa pekee yao. Kwa upande wao, sasa wananchi wameamua, kuungana dhidi wabunge na rais.
Muungano huo umesema jukwaa hili la kidijitali, ni nyongeza na juhudi zingine kama vile raia kususia ushuru kwa kusudi la kuilazimisha serikali kufutilia mbali mswada wa fedha wa 2023 na kuchukua hatua za makusudi za kupunguza gharama ya maisha.
Akizungumza na waandishi wa habari, Raila amesema vitendo hivi pia vinakusudiwa kushurutisha utawala wa Kenya Kwanza kushughulikia masuala yote mazito ambayo wamekuwa wakisisitiza, ikiwa ni pamoja na uundaji upya wa tume ya uchaguzi IEBC unaohusisha pande zote mbili na ukaguzi wa uchaguzi wa 2022.
Akirejelea maandamano ya wiki iliyopita akitoa madai ya mauaji dhidi yake, Raila amesema kama vile mauaji ya Martin Luther King, Jr. au kuwekwa kizuizini kwa Nelson Mandela na Mahatma Gandhi havikuzuia maandamano ya haki za kiraia na uhuru nchini Marekani, Afrika Kusini na India, hakuna kiasi cha risasi, machozi au hata mauaji yatakomesha maandamano ya historia nchini Kenya.
Hata hivyo, tunanuia kuenda mahakamani na kuanzisha mashtaka dhidi ya maafisa wa polisi walioenda kinyume cha sheria dhidi ya waandamanaji wiki iliyopita. Shughuli zetu zinalindwa na katiba.
Kadhalika, Raila amesisitiza kuwepo kwa maandamano Jumatano, Julai 12 yatakayofanyika katika uwanja wa Kamkunji jijini Nairobi.
Nataka wakenya wote kila mahali wafuasi wa Azimio na hata wale wa Kenya Kwanza wajitokeze ili kuonyesha kuwa punda amechoka.
Haya yakijiri hapo jana, mahakama kuu nchini Kenya iliongeza muda wa mswada wa fedha kutoanza kutekelezwa baada ya kufutiia mbali ombi la serikali la kuondoa kizuizi hicho.
Naye rais Ruto amesema wale ambao wanapanga maandamano wamekasirishwa na hatua yake ya kutaka kuwapa vijana kazi.