Kenya: Upinzani kuendelea na maandamano kushinikiza kushuka kwa gharama ya maisha
Nairobi – Nchini Kenya, polisi wametumia mabomu ya machozi, kupambana na maelfu ya waandamanaji, jijini Nairobi na katika miji mingine, waliojitokeza kulalamikia sera za rais William Ruto zilizosababisha kupanda kwa gharama ya maisha.
Imechapishwa:
Wakiongozwa na kiongozi wa upinzani Raila Odinga, waandamanaji walijaribu kufika katika viwanja vya Uhuru Park katikati mwa jiji, lakini polisi walitumia maji ya kuwasha kuwasambaratisha.
Kabla ya hapo Odinga alikutana na waandamanaji katika viwanja vya kihistoria vya Kamukunji Mashariki mwa jiji la Nairobi, na kuanza harakati wa kukusanya saini Millioni 10 dhidi ya serikali ya Ruto.
"Mimi mwenyewe nitaanza hapa hapa kuweka saini na kila kitu ambacho tutafanya tutakifanya kwa njia ya amani." alisema Odinga.
Raila Odinga, Kinara wa upinzani nchini Kenya
Maandamano haya yamefanyika katika miji mingine kama Mombasa na Kisumu. Hawa ni baadhi ya waandamanaji.
"Maisha yamekuwa magumu sana tunataka mabadiliko." alisema mmoja wa waandamanaji.
Baadhi ya waandamanaji nchini Kenya
Siku chache zilizopita, rais Ruto alitia saini sheria iliyoongeza kupanda kwa kodi na kusababisha kupanda kwa bei ya mafuta. Ruto amekuwa akitetea uamuzi wake.
"Hakuna namna ambayo unaweza kumuinua mtu wa chini kabla hujampangia vile atakuwa na pesa kwa mfuko." alisema rais Ruto.
Rais wa Kenya, William Ruto
Waandamanaji wametumia siku maarufu ya saba saba, kukumbuka harakati za miaka ya tisini wakati maandamano makubwa yalifanyika siku kama hii, kudai siasa za vyama vingi, kushinikiza madai yao dhidi ya serikali ya Ruto.