Uganda: Washukiwa watatu wa shambulio dhidi ya shule wamekamatwa
NAIROBI – Mamlaka nchini Uganda imethibitisha kukamatwa kwa watu watatu wanaohusishwa na shambulio katika shule ya Lhubiria nchini humo Ijumaa iliyopita ambapo watu 40 waliauwa.
Imechapishwa:
Idadi kubwa ya walioauwa katika shambulio hilo la kigaidi katika mji wa Mpondwe Magharibi wa taifa hilo walikuwa ni wanafunzi.
Wengi wao walichomwa hadi kufa wakati wakiwa katika bweni lao la kulala.
Kwa mujibu wa mkuu wa wilaya Joe Walusimbi, hatua ya kukamatwa kwa washukiwa hao imefanikishwa baada ya raia kutoa taarifa kwa maofisa wa usalama.
Kando na kutekeleza mauaji hayo, waasi hao wanaoendeleza shughuli zao mashariki mwa DRC, wametuhumiwa kwa kuwateka wanafunzi sita kabla ya kuvuka mpaka na kuingia nchini DR Congo.
Rais wa Uganda Yoweri Museveni, amelaani shambulio hilo ambalo amelitaja kuwa la kioga.
Licha ya kukamatwa kwa watatu hao, jeshi nchini humo linaendelea na shughuli za kuwasaka waasi wa kundi la ADF wanaodhaniwa kuwa wametorokea katika nchi jirani ya DRC.
ADF wamekuwa wakituhumiwa kwa kutekeleza mashambulio dhidi ya raia katika eneo la mashariki ya Jamhuri ya kidemokrasia ya kongo.