Kenya: Upinzani watoa masharti mapya ya mazungumzo na Serikali
NAIROBI – Kiongozi wa upinzani nchini Kenya, Raila Odinga, wiki hii ametoa masharti mapya ya mazungumzo na Serikali, sasa akitakata mazungumzo hayo yasichukue zaidi ya siku 30, matamshi anayotoa siku chache baada ya kuarisha tena kwa muda maandamano.
Imechapishwa:
Kupitia taarifa iliyosomwa na Eugene Wamalwa, moja ya viongozi wa muungano wa Azimio, alisisitiza upande wao kutokuwa na nia yoyote ya kupewa nafasi za uongozi katika Serikali iliyopo madarakani.
“Tumewaelekeza wajumbe wetu wawe wazi kwamba hatuwezi kuendelea na mazungumzo haya kwa zaidi ya siku 30 tangu yatakapoaanza.” Alisema Eugene Wamalwa.
Eugene Wamalwa, kuhusu Mazungumzo na kisiasa nchini Kenya
Aidha muungano huo pia unataka serikali kuwaachia huru bila masharti vijana wanaoegemea mrengo huo ambao walikamatwa wakati wa maandamano ya awali.
Azimio la Umoja inasema kwamba wafuasi wake walikamatwa na kufikishwa mahakamani wakikabiliwa na kesi za kugushi wakiwatuhumu maofisa wa polisi kwa kuwazuilia licha wao kutoa taarifa kwa vyombo vya usalama kwamba watafanya maandamano.
Polisi wamekuwa wakiwatuhumu wafuasi wa mrengo huo kwa kutekeleza uharibifu wa mali ya raia wakati wa maandamano ya awali ambayo baadhi ya wafanyabishara walithibitisha kuporwa mali yao.
Licha ya madai hayo ya polisi, Azimio imendelea kudai kuwa wafuasi wao hawakuhusika na uporaji na uharibifu wa mali wakiituhumu serikali kwa kukodi wahuni waliotekeleza uharibifu huo wa mali.
Kwa sasa, raia katika taifa hilo la Afrika Mashariki wanasubiri kuona iwapo mazungumo kati ya upinzani na serikali yatazaa matunda na kutatua mvutano wa kisiasa uliopo kwa sasa.
Katika hatua nyingine, viongozi hao wamesema ikiwa mazungumzo wanayotarajia kuanza hayazaa matunda, watalazimika kurejea tena barabarani.