Kenya: Vurugu zatawala maandamano ya upinzani
NAIROBI – Vurugu zimeripotiwa siku ya Alhamisi, katika baadhi ya maeneo nchini Kenya, ikiwa ni katika siku ya tatu ya maandamano yaliyoitishwa na upinzani, dhidi ya serikali kupinga kupanda kwa gharama ya maisha. Kama ilivyokuwa juma lililopita, kinara wa Azimio Raila Odinga aliungana na wafuasi wake.
Imechapishwa:
Msafari wa muungano wa Azimio la Umoja One Kenya ukiongozwa na Raila Odinga uliingia katika mtaa wa Imara Daima, katika eneo bunge la Embakasi, kisha mtaa wa mabanda wa Mukuru kwa Njenga, ambapo katika kila hatua kiongozi huyo amesisitiza kuendelea na maandamano, licha ya serikali kusema maandamano hayo si halali.
Odinga, amewaagiza wafuasi wake kuandamana kila wiki, siku ya Jumatatu na Alhamisi, kuipinga serikali tawala inayoongozwa na rais William Ruto na kulalamikia gharama ya juu ya maisha ambayo inashuhudiwa kote nchini.
Hata wafanye nini, walete maaskari milioni moja, Kenya iko na nguvu zaidi, nguvu ya siasa ni ya wananchi, je mnaunga mkoni Azimio? Amesema RailaKinara wa upinzani nchini Kenya, Raila Odinga
Katikati ya jiji la Nairobi, hali ilikuwa ile ile ya biashara kufungwa, usafiri kuathirika na vikosi vya polisi kushika doria, baadhi ya wananchi wakilalamikia hali hii.
Jina langu ni James Oyoo, mimi ni mfanyakazi wa halmashauri ya usafiri ilhali usafiri iko chini kwa sasa, mimi ningeomba wakenya wakubaliane na hali yenye iko, tuishi vile kuko, tununue hiyo bidhaa vile zinauzwa na hiyo bei bora mapato yetu iiingie ya kila siku.Raia James Oyoo akiwa jijini Nairobi
Maandamano pia yalishuhudiwa katika kaunti za Migori, Homabay na vilevile Kisumu, ambapo pia polisi walikabiliana na waandamanaji, huku baadhi ya raia wakiomba viongozi walio madarakani kuwa na maelewano.
Tungeomba kwamba mheshimiwa Raila Amollo Odinga, hii mambo ya maandamano waelewane na mheshimiwa rais Ruto, ndio tuone vile tunaendelea kwenda mbele, sisi watu wa Nyanza tulinufaika kutokana na mapatanao ya awali, barabara zilitengenezwa, nawaomba pia ndugu zetu kutoka Nyanza wasiharibu mali yao. Amesema raia huyo.Raia jijini Kisumu, nchini Kenya
Odinga amesema yeye na wafuasi wake ni wakenya wazalendo, na wataendelea na maandamano hadi pale serikali itakaposikia kilio cha mwananchi wa kawaida na kushughulikia maswala ibuka.