Côte d'Ivoire yafungua tena mipaka yake ya ardhini
Kufunguliwa tena kwa mipaka ya ardhini kunaanza kutekelezwa Alhamisi asubuhi. Mipaka ya Côte d'Ivoire ilikuwa imefungwa tangu Machi 22, 2020 ili kukabiliana na kuenea kwa mlipuko wa Uviko-19.
Imechapishwa:
Kufungwa kwa mipaka ya ardhini, hatua iliyokuwa ikitumika kwa karibu miaka mitatu sasa imeondolewa, kwa sababu ya "maendeleo mazuri ya kiafya na kiuchumi", limebaini Baraza la Mawaziri. Tayari mwezi uliopita, Baraza la Usalama la Kitaifa lilitangaza kuondolewa hatua kwa hatua kwa hatua hizi za kuzuia kuenea kwa maambukizi ya virusi vya Corona.
Uamuzi huu unalenga kukomesha njia sisizo kuwa rasmi na kuwaelekeza wasafiri kwenye vivuko rasmi. Kwa sababu hadi wakati huo, watu walikuwa wakitumia njia zisizo rasmi, kulingana na wakazi kadhaa wa Ouangolodougou, mji ulio karibu na mpaka na Burkina Faso. "Hii itawezesha kuelekezwa upya kwa watu kwenye kutumia vivuko rasmi, ili kuhakikisha udhibiti bora wa wimbi la wahamaji," ameelezea Amadou Coulibaly, msemaji wa serikali. Kikao cha mwisho cha Baraza la usalama la kitaifa lilibainisha "wimbi la hivi majuzi" la wakimbizi 8,700 wa Burkina Faso waliokimbia ghasia nchini mwao. Mamlaka ya Côte d'Ivoire inataka kuwatambua na kuanzisha maeneo ya mapokezi.
Kufunguliwa tena kwa mipaka ya ardhini pia ni afueni kwa wachukuzi ambao shughuli zao zimepungua sana katika miaka ya hivi karibuni. Muungano wa Madereva wa Malori wa Afrika Magharibi (Ucrao), unaojumuisha karibu kampuni 300 za usafirishaji, umesema uko tayari kurejesha hatua kwa hatua shughuli zake. "Lazima tujaze nguvu kazi katika vituo vya mabasi, kwa sababu madereva walikuwa wamejikuta hawana ajira", anaeleza Daouda Bamba, katibu mkuu wa muungano huo. Karibu madereva na wasaidizi wao 24,000 wanatarajia kurejea kazini, kulingana na Daouda Bamba.