Miji kadhaa yakumbwa na maandamano DRC
Mamia ya watu wameandamana Ijumaa hii mchana katika mji wa Kinshasa, kufuatia wito wa vyama kadhaa vya upinzani ,kupinga matumizi ya mashine za kupigia kura wakati wa uchaguzi Mkuu nchini humo.
Imechapishwa:
Vyama vya upinzani vinapinga pia marekebisho ya fomu ya uchaguzi inayotajwa kuwa "imepitwa na wakati" kwa uchaguzi wa urais uliopangwa kufanyika Desemba 23. Hata hivyo, chama cha UDPS, moja ya vyama vikuu vya upinzani, hakikubaliani na utaratibu uliotumiwa na vyama vingine vya upinzani kwa maandamano hayo. Gavana wa mkoa wa Kinshasa alikubali maandamano hayo yafanyike kwa sharti kuwa ratiba ibadilishwe. Waandamanaji hawakuruhusiwa kwenda kwenye makao makuu ya tume ya uchaguzi kama walivyotamani.
Maandamano yalianza saa 12h asubuhi na yalifanyika kwa utulivu kabla ya kuhiutimishwa kwenye eneo la Triomphale. Polisi ilizingira kwa umbali msafara wa waandamanaji na kwenye barabara kuu ya Lumumba, ambapo shughuli zimeendelea kama kawaida, maandamano yalifanyika.
Miongoni mwa viongozi wa kisiasa wa upinzani katika maandamano hayo, ni pamoja na Martin Fayulu, Vital Kamerhe aliyerejea nchini jana Alhamisi usiku kutoka Afrika kusini. Kulikuwepo pia pAdolphe Muzito, Fidelel Babala wa chama cha MLC cha Jean-Pierre Bemba. Hata hivyo mwenyekiti wa chama cha MLC Jean_Pierre Bemba hakushiriki maandamano hayo. Chama chake hakijatoa maelezo rasmi.
Kama kilivyotangaza hapo awali, chama cha UDPS hakikushiriki katika maandamano kikitaja kuwa malengo ya maandamano hayo yalikuwa "hayaeleweki", amesema Jean-Marc Kabund, katibu mkuu wa chama cha UDPS.
Katika mji wa Lubumbashi kulitokea makabiliano kati ya jeshi na waandamanaji.
Katika mji wa Mbuji-Mayi, vikosi vya usalama vilisambaratisha maandamano hayo, licha yakuwa waandamanaji walikuwa na kibali kinachowaruhusu kufanya kampeni.
Katika miji ya Kisangani na Bukavu, hakuna maandamano yoyote yaliyoshuhudiwa.