Hatima ya Bemba kuachiwa au la kujulikana Jumanne hii
Siku chache tu zikiwa zimepita tangu majaji katika mahakama ya kimataifa ya uhalifu wa kivita ya ICC wamfutie makosa ya uhalifu wa kivita na dhulma dhidi ya binadamu makamu wa rais wa zamani wa DRC Jean-Pierre Bemba, leo mahakama hiyo itatoa uamuzi ikiwa Bemba ataachiwa huru au la.
Imechapishwa:
Hata hivyo wataalamu wa masuala ya sheria za kimataifa wanasema kunau wezekano mkubwa kiongozi huyo wa zamani wa kivita kuachiwa huru.
Ofisi ya mwendesha mashitaka ya ICC ilishindwa kutoa ushahidi tosha unaomuhusisha Bemba katika uhalifu uliotekelezwa na wapiganaji wake nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati.
Jean-Pierre Bemba mwenye umri wa miaka 55 alikataa rufaa mwezi Juni 2016 kwa uamuzi wa ICC kumpata na kosa la kuhusika katika mlolongo wa mauaji na ubakaji, vitendo vilivyofanywa na wanamgambo wake wa kundi la waasi la MLC, nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati kati ya mwezi Oktoba 2002 na mwezi Machi 2003.
Katika muda wa miezi mitano, wapiganaji 1,500 wa MLC waliua, waliiba na kubaka nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, ambapo walikwenda kumsaidia rais Ange-Félix Patassé dhidi ya jaribio la mapinduzi lililoendeshwa na Jenerali François Bozizé.
Kesi yake iliyofunguliwa mjini Hague mnamo mwezi Novemba 2010, ilikuwa ni ya kwanza ya ICC iliyolenga ubakaji na unyanyasaji wa kijinsia kama uhalifu wa kivita na kumuhusisha kiongozi mkuu wa jeshi kutokana na uzembe kwa watu waliokua chini ya uongozi wake
Hukumu ya kifungo cha miaka 18 ni hukumu kubwa kabisa kuwahi kutolewa na mahakama hiyo ilianzishwa mwaka 2002 ili kuhukumu uhalifu mbaya unaotekelezwa duniani.