Urusi: Familia ya Navalny yaomba kukabidhiwa mwili wake mara moja
Timu ya kiongozi wa upinzani nchini Urusi na mkosoaji mkuuu wa Kremlin Alexeï Navalny aliyeripotiwa kufariki akiwa jela siku ya Ijumaa, inaomba mwili wake ukabidhiwe familia yake "mara moja", baada ya mamake mwanaharakati huyo kufahamishwa rasmi kuhusu kifo chake gerezani.
Imechapishwa:
"Mfanyakazi katika jela alikokuwa anazuiliwa kiongozi huyo wa upinzani amesema kuwa mwili wa Alexei Navalny ulikuwa Salekhard," mji katika eneo la Urusi la Arctic ambapo alikuwa akizuiliwa, na ulichukuliwa na "wachunguzi" kwa "kufanya 'utafiti'", amebainisha Kira Iarmich, msemaji wa Alexei Navalny.
"Tunaomba mwili wa Alexeï Navalny ukabidhiwe mara moja kwa familia yake," ameongeza, akibainisha kuwa wakuu wa mamlaka ya gereza walimpa mama yake, Lyudmila Navalanïa, hati "rasmi" kuthibitisha kifo cha mwanae.
Ndugu wa karibu wa Navalny wamesema, ni wazi kuwa, serikali ya Urusi inagoma kuwapa mwili huo kwa sababu wanajaribu kuficha ushahidi muhimu kuhusu kilichosababisha kifo chake.
Hata hivyo, ripoti zinasema serikali jijini Moscow imesema itakabidhi mwili huo baada ya uchunguzi kukamilika kubaini kilichomuua.
Kifo cha Navalny, kimelaaniwa na viongozi mbalimbali wa nchi za Magharibi wakiongozwa na rais wa Marekani Joe Biden, ambaye amemshtumu rais Putin kuhusika na kufariki kwa mpinzani wake, aliyekuwa amefungwa jela kwa makosa ambayo yameelezwa kuchochewa kisiasa.