UVIKO-19: Baadhi ya nchi za EU zaingiliwa na wasiwasi juu ya wasafiri kutoka China
China imetangaza kusitishwa kwa hatua zake za kukabiliana na ugonjwa hatari wa UVIKO na kufungua tena mipaka yake. Kwa hivyo wasafiri kutoka China wataweza tena kusafiri nje ya nchi. Na hii inasababisha wasiwasi mkubwa katika baadhi ya nchi za Umoja wa Ulaya.
Imechapishwa:
Wakati Italia imejikuta ikiwa na idadi kubwa ya watalii kwa Sikukuu hizi za Mwisho wa Mwaka, viongozi wa afya, wakishtushwa na kuondolewa kwa vizuizi nchini China, wameamua kuwapa wasafiri wote kutoka nchi hii vipimo vya antijeni. Tangu Desemba 26, karibu watalii 100 wa China, kati ya 210 ambao tayari wamewasili kwenye uwanja wa ndege wa Milan Malpensa, wamepimwa na kukuta wameambukizwa virusi vya Corona vinavyosababiha ugonjwa wa UVIKO-19, anaripoti mwandishi wetu huko Roma, Anne Le Nir. Kwa hivyo, serikali ya Italia imeamua kufanya vipimo vya haraka vya antijeni kuwa vya lazima kwa wasafiri wote wanaowasili kutoka China, pamoja na wale wanaosafiri kuelekea nchi zingine wakipitia nchini Italia.
Kulingana na Waziri wa Afya, Orazio Schillaci, hatua hii ni muhimu ili kuhakikisha ufuatiliaji na utambuzi wa aina mpya zinazowezekana za virusi, ili kulinda raia wa Italia. Waziri wa Afya amebainisha kuwa alikuwa akiwasiliana na mamlaka husika za nchi nyingine wanachama wa Umoja wa Ulaya ili kufafanua mkakati wa pamoja.
Ufaransa kujadili hatua zote muhimu
Serikali ya Ufaransa, kwa upande wake, inahakikisha "kufuatilia kwa makini sana mabadiliko ya hali nchini China". Siku ya Jumatano, Desemba 28, Waziri wa Afya alisema yuko "tayari kujadili hatua zote muhimu ambazo zinaweza kutekelezwa, kwa kushirikiana na washirika wa Ufaransa wa Ulaya, na ndani ya mfumo wa kisheria uliopo leo".