Mmoja kati ya viongozi wa waasi nchini Ukraine akamatwa
Mawaziri wa mambo ya nje wa nchi za Ujerumani, Ufaransa, Urusi na Ukraine wanakutana leo mjini Berlin, nchini Ujerumani, katika jitihada za kutafutia suluhu mzozo unaoendelea nchini Ukraine, siku moja baada ya serikali ya Kiev kuanzisha operesheni ya kijeshi dhidi ya waasi.
Imechapishwa:
Hayo yanajiri wakati katibu mkuu wa jumuiya ya kujihami ya mataifa ya magharibi NATO, Anders Fogh Rasmussen amekutana kwa mazungumzo na waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani, Frank-Walter Steinmeier, na baadae kansela wa Ujerumani Angela Merkel.
Mazungumzo ya viongozi hao yamegubikwa na mzozo unaoendelea nchini Ukraine. Vingozi hao wamekua wanasubiriwa kutoa taarifa ya pamoja na kuendesha mkutano na waandishi wa habari hii leo mchana.
Wakati huohuo rais wa Urusi Vladimir Poutin amejielekeza katika mji wa MINSK nchini Belarus kusheherekea maadhimisho ya miaka 70 ya taifa hilo kujitenga na Urusi na kuwa taifa huru
Wakati hayo yakijiri, kikosi maalum cha Ukraine kimefahamisha jumatano hii kwamba kimemkamata mmoja kati ya viongozi wa wa wanaharakati wa mashariki mwa Ukraine waliyojitenga. Kwa mujibu wa kikosi hicho, kiongozi huyo amekamatwa wakati alipokua akijaribu kuulizia bei ya silaha nzito za kijeshi pamoja na silaha zingine ndani ya mgahawa moja katika mkoa wa wa Zaporijjia(kusini mashariki).
Volodymyr Kolosniouk, ambaye ni meya wa mji wa Gorlovka, moja ya maeneo muhimu ya wanaharakati katika mkoa wa Donetsk, alikua afisa anaehusika na kuhifadhi silaha za wapiganaji wa mji huo, ambao walikua wakiongozwa na kiongozi wa waasi Igor Bezler, kwa jina maarufu Bies (pepo mbaya kwa lugha ya Ukraine), ambae alipata mafunzo ya kijeshi ya hali ya juu, kimeendelea kusema kikosi hicho maalumu katika taarifa kiliyotoa.
Volodymyr Kolosniouk anakabiliwa na tuhuma za kuunda na kufadhili kundi la kigaidi. Anashukiwa kushiriki katika mashambulizi mbalimbali dhidi ya jeshi la Ukraine lililoanzisha “operesheni dhidi ya ugaidi” huko mashariki mwa nchi.