DRC: Volcano ya Nyiragongo yalipuka, wakaazi wa Goma wahama mji
Maelfu ya wakazi wa mji wa Goma wamelazimika kuyahama makazi yao kufuati mlipuko wa Volcano maarufu ya Nyiragongo, karibu na jiji hilo, mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC). Mlipuko huo ulianza kuripotiwa jana Jumamosi jioni.
Imechapishwa:
Serikali nchini Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo imeagiza watu waondolewe kutoka mji wa mashariki wa Goma, baada ya kutokea mlipuko huo wa volcano katika mlima Nyiragongo uliopo karibu na mji huo wa mpakani.
Rais Tshisekedi, ambaye kwa sasa yuko Ulaya, ametangaza kurudi nchini Jumapili "ili kusimamia uratibu wa misaada kwa watu wa eneo hilo".
Mlipuko huo wa Volkano Nyiragongo ulianza kuripotiwa saa moja usiku saa za Afrika ya Kati.
Raia waamua kukimbilia maeneo salama
Raia wengi wamekimbilia katika nchi jirani ya Rwanda na wengine walielekea magharibi kwenye mji wa Sake uliopo kwenye jimbo la Masisi la nchi jirani ya Jamuhuri ya Congo.
Afisa mmoja katika hifadhi ya kitaifa ya Virunga iliyopo kwenye eneo ambako volcano imelipuka amesema hadi hii leo asubuhi tope la moto linalotiririka kutoka kwenye mlima Nyiragongo limefika kwenye uwanja wa ndege wa mji huo wa Goma na kwamba hali inazidi kuwa mbaya.
Afisa huyo amesema anahofia kwamba tope hilo la moto (Lava) linaweza kufika hadi kwenye fukwe za ziwa Kivu. Amesema mlipuko huo unalingana na ule uliotokea mwaka 2002 na amewataka raia waondoke mahala hapo haraka.