UN yasema Al Shabab bado tishio nchini Somalia
Umoja wa Mataifa umeonya kuwa Kundi la Al Shabaab la nchini Somalia bado lina uwezo wa kuzindua mashambulizi kwa kiasi kikubwa licha ya madai kuwa uasi wa kundi hilo umedhoofishwa.
Imechapishwa:
Kundi hilo la kiislam limetekeleza mashambulizi mabaya sita katika hotel mjini Mogadishu Somalia tangu mwezi Novemba mwaka 2015 hadi mwezi Juni mwaka huu, ripoti ya waangalizi wa vikwazo wa Umoja wa mataifa imeeleza jana Ijumaa.
Waangalizi hao wamesema kuwa kinyume na taarifa zilizopo za mafanikio katika kukabiliana na uasi na ugaidi,hali ya usalama haijaboreka nchini Somalia.
Kundi la Al Shabaab linaweka tishio zaidi kwa amani na usalama nchini Somalia na linaendelea kuzorotesha amani na usalama katika eneo kubwa la Mashariki na Pembe ya Afrika,imeongeza ripoti ya Baraza la Usalama mapema wiki hii.
Wakati kundi hilo likiwa halijafanya mashambulizi makubwa nje ya Somalia tangu mauaji ya mwaka 2015 katika Chuo Kikuu cha Garissa Kenya,kundi hilo limeendelea kuwa na uwezo wa kufanya shambulio lingine la aina hiyo njia ambayo linaitumia kujitangaza katika kulenga nchi zinazochangia askari wa AMISOM.
Kikosi cha umoja wa Afrika AMISOM nchini Somalia kinajumuisha askari wengi kutoka Kenya, Ethiopia, Uganda na Burundi.