Ufaransa yaweka kipimo cha PCR kwa msafiri yeyote anayewasili kutoka nchi isiyo ya EU
Wasafiri wanaowasili nchini Ufaransa kutoka katika nchi ambayo si mwanachama wa Umoja wa Ulaya sasa watalazimika kuwasilisha cheti kinachoonyesha kuwa walifanya kipimo cha PCR, na kukutwa hawana maambukizi yoyote ya virusi vya Corona , ikiwa wamechanjwa au la.
Imechapishwa:
Kutokana na tishio la kirusi kipya cha Omicron, Ufaransa imetangaza Jumatano hii, Desemba 1 kwamba inaongeza masharti ya kuingia kwenye ardhi yake kwa kuweka hasa kipimo kinachoonyesha kuwa wasafiri wote hawana maambukizi ya virusi vya Corona, hata kama walichanjwa, na ambao wanatoka katika si mwanachama wa Umoja wa Ulaya. Kwa wasafiri kutoka nchi za Umoja wa Ulaya, Ufaransa itaweka kipimo cha saa 24 kwa watu ambao hawajachanjwa.
Msemaji wa serikali ya Ufaransa Gabriel Attal pia ametangaza kwamba safari za ndege na nchi kumi za kusini mwa Afrika zitaanza tena kuanzia Jumamosi, Desemba 4, lakini kwa "usimamizi mkali". Raia wa Ufaransa, raia wa Umoja wa Ulaya, wanadiplomasia na wasafiri wa baharini pekee ndio wataweza kusafiri kwenda maeneo haya. Wasafiri hawa pia watapimwa Covid watakapowasili Ufaransa, ikifuatiwa na kuwekwa karantini kwa siku saba ikiwa hawatakutwa na maambukizi ya virusi na siku kumi ikiwa watapatikana na maambukizi ya virusi, amesema Gabriel Attal.
Faini kutozwa kwa watu ambao hawataheshimu sheria
Katika visa vyote viwili, karantini "itafuatiliwa na vikosi vya usalama waa ndani na ikiwa karantini haitaheshimishwa, faini ya euro 1,000 hadi 1,500" itatozwa, ameongeza msemaji huyo.
Hatua hizi zinahusu nchi saba ambazo safari za ndege zilisitishwa tangu Ijumaa, Novemba 26 (Afrika Kusini, Lesotho, Botswana, Zimbabwe, Msumbiji, Namibia na Eswatini), na nchi za Malawi, Zambia na Mauritius, ambazo zimeongezwa.