Wagombea wenza nchini Kenya kuchuana katika mdahalo wa runinga
Mdahalo wa wagombea wenza nchini Kenya, kuelekea Uchaguzi Mkuu mwezi ujao umepangwa kufanyika katika Chuo Kikuu cha Katoliki cha Afrika Mashariki leo jioni jijini Nairobi.
Imechapishwa:
Wakenya wanasubiri mchuano mkali kati ya Naibu rais wa sasa William Ruto ambaye ni mgombea mwenza wa rais Uhuru Kenyatta anayetafuta urais kwa muhula wa pili na mpinzani wake Kalonzo Musyoka, mgombea mwenza na mgombea urais wa upinzani NASA Raila Odinga.
Hata hivyo, kuelekea mdahalo huu utakaopeperushwa kupitia vyombo vya Habari nchini humo, kuna wasiwasi ikiwa wagombea wenza hao wawili watashiriki baada ya William Ruto kusema kuwa hakufahamishwa kuhusu mdahalo huu.
Kalonzo Musyoka naye hajaeleza iwapo atakuwepo katika mdahalo huo ambao utaanza saa mbili na nusu usiku saa za Afrika Mashariki na kumalizika saa tatu na nusu.
Waandaji wa mdahalo huo wanasema maandalizi yote yamekamilika, kupeperusha mdahalo huo moja kwa moja.
Mdahalo wa kwanza unaowaleta pamoja wagombea wenza wengine sita, unatarajiwa kuanza saa kumi na moja na nusu jioni.
Wagombea wenza hao ni pamoja na Eliud Kariara, Emmanuel Nzai, Joseph Momanyi, Miriam Mutua, Titus N'getuny na Moses Maranga.
Mdahalo wa wagombea urais unatarajiwa kufanyika baadaye mwezi huu kati ya wagombea wote nane, huku wagombea wakuu wakiwa ni rais Uhuru Kenyatta na Raila Odinga.