Kenya: Sita wauawa katika shambulio la Al Shabaab Lamu
Watu sita wameuawa na vijiji kuchomwa moto na watu wanaoshukiwa kuwa wanamgambo wa Al Shabab katika mji wa pwani wa Lamu nchini Kenya.
Imechapishwa:
Kamishna wa Kaunti ya Lamu Irungu Macharia amesema watu sita wameuawa na nyumba zimechomwa moto katika shambulio la hii leo linaloshukiwa kufanywa na wanamgambo wa Al-Shabaab.
Kamishna Irungu Macharia amesema vikosi vya usalama vinafuatilia matukio hayo na amewaomba wenyeji kutoa ushirikiano.
Wapiganaji wa Al-Shabaab wamefanya mashambulizi kadhaa makubwa ndani ya Kenya kulipiza kisasi kutokana na serikali ya nchi hiyo kuwapeleka wanajeshi wake nchini Somalia mnamo mwaka 2011 kama sehemu ya kikosi cha Umoja wa Afrika.
Kundi hilo linaloshirikiana na mtandao wa Al Qaeda linataka kuiondoa madarakani serikali ya mjini Mogadishu inayoungwa mkono kimataifa.