Zambia yafanya uchaguzi licha ya kudorora kiuchumi
Wapiga kura milioni saba nchini Zambia wanamchagua leo Alhamisi rais wao na wabunge, katika uchaguzi uliogubikwa na ghasia za kabla ya uchaguzi na kupelekwa kwa idadi kubwa jeshi katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Imechapishwa:
Wagombea kumi na sita watapambana katika uchaguzi wa urais, lakini wawili ndio wanapewa nafasi kubwa katika uchaguzi huo: rais anayemaliza muda wake Edgar Lungu, wa chama cha Patriotic Front, na Hakainde Hichilema, wa chama cha United Party for National Development (UPND), ambaye anawania mara ya sita.
Edgar Lungu na Hakainde Hichilema watachuana Alhamisi kwa mara ya tatu.
Edgar Lungu, aliyechaguliwa katika uchaguzi uliozua utata mwaka 2016, sasa anawania muhula wa pili. Mpinzani wake mkuu, Hakainde Hichilema, amekamatwa mara kadhaa tangu atangaze kugombea urais.
Mnamo mwezi Juni, shirika lisilo la kiserikali la Amnesty International tayari lilionyesha ukandamizaji "wa kikatili" uliofanywa na rais Edgar Lungu dhidi ya wapinzani wote, na kuitaja Zambia kama nchi "ambapo haki za binadamu ziko katika mgogoro".
Angalau watu watatu waliuawa katika makabiliano kati ya wafuasi mwishoni mwa juma lililopita. Vurugu hizo zilisababisha kupelekwa kwa jeshi katika maeneo mbalimbali nchini humo Agosti 1.
Hivi karibuni Maaskofu nchini Zambia walitoa wito kwa raia wote kupiga kura kwa amani na kuepuka vurugu ili kufikia malengo ya kisiasa.