Wanafunzi waliotekwa, nchini Nigeria, waachiliwa huru
Raia 42 waliokuwa wametekwa na kundi la watu wenye silaha katika jimbo la Niger, nchini Nigeria, wakiwemo wanafunzi 27 wameachiliwa huru, gavana wa jimbo hilo, Abubakar Sani Bello ,amethibitisha.
Imechapishwa:
Ni kisa kinachojiri siku moja baada ya kundi jingine la watu wenye silaha kuteka wanafunzi 300, katika jimbo la Zamfara.
Visa hivi vinadaiwa kuongezeka kaskazini mwa taifa la Nigeria, kutokana na hatua ya makundi hayo kupewa pesa ili kuwachilia huru raia wanaowateka.
Utekaji nyara umeibua wasiwasi kuhusu usalama wa raia nchini humo, makundi ya kijahidi ya Boko Haram na lile ya Islamic State, yakiwa baadhi ya makundi ambayo yamekuwa yakitumia mbinu hiyo.
Swala usalama limesalia changamoto kwa serikali ya rais Muhammadu Buhari, mwanajeshi mustaafu, na ambaye amekuwa akishtumiwa kwa kushindwa kudhibiti makundi ya wanajihadi.
Mapema mwezi huu rais Buhari, alilazimika kubadilisha mkuu wa jeshi nchini humo, ili kusaidia kukabili wanajihadi hao.