Joto la kisiasa laendelea kufukuta kuelekea uchaguzi wa urais Ufaransa
Nchini Ufaransa, rais wa zamani Nicholas Sarkozy alizomewa jana na wafuasi wa chama cha Republican, baada ya kutoonekana kumfanyia kampeni mgombea wa urais Valerie Pecresse.
Imechapishwa:
Hatua hii ya wafuasi wa chama hicho cha mrengo wa kulia, imekuja baada ya Sarkozy kukataa kumuunga mkono Pecresse, aliyehudumu kama Waziri wake wa Bajeti, wakati alipokuwa rais kati ya mwaka 2007-2012.
Wafuasi wa Republican wamekasirishwa na hatua ya Sarozy kutokuwa karibu na mgombea wao Pecresse na badala yake kuonekana kumkumbatia rais wa sasa Emmanuel Macron anayetafuta muhula wa pili, na Jumamosi iliyopita, alifanya mkutano mkubwa wa siasa jijini Paris kuomba kuchaguliwa tena.
Kura za maoni zinaonesha kuwa Pecresse huenda akamaliza wa nne au wa tano kwenye uchaguzi wa urais utakaofanyika siku ya Jumapili, huku ushindani mkali ukitarajiwa kati ya rais Macron na Marine Le Pen ambao wameonekana kuchuana vikali.
Kampeni nchini Ufaransa zimeingia katika mkono wa lala salama, kuelekea siku ya Jumapili, na iwapo mshindi hatapata asilimia 50 ya kura, kutakuwa na duru ya pili Aprili 24.