Pata taarifa kuu
UFARANSA-NICOLAS SARKOZY

Ufaransa: Sarkozy ahojiwa na polisi kwa tuhuma za kupokea fedha toka kwa Gaddafi

Rais wa zamani wa Ufaransa Nicolas Sarkozy Jumanne ya wiki hii amezuiliwa na kuhojiwa na polisi kuhusu tuhuma kuwa alipokea fedha kufadhili kampeni zake za urais kwenye uchaguzi wa mwaka 2007 kutoka kwa rais wa zamani wa Libya marehemu Kanali Muamar Gaddafi.

Aliyekuwa rais wa Ufaransa, Nicolas Sarkozy (kulia) akiwa na aliyekuwa rais wa Libya, Muammar Gaddafi wakiwa Paris, Desember 10, 2007.
Aliyekuwa rais wa Ufaransa, Nicolas Sarkozy (kulia) akiwa na aliyekuwa rais wa Libya, Muammar Gaddafi wakiwa Paris, Desember 10, 2007. REUTERS/Patrick Hertzog/Pool/File Photo
Matangazo ya kibiashara

Sarkozy alizuiliwa asubuhi ya siku ya Jumanne na kuhojiwa na waendesha mashtaka waliobobea kwenye masuala ya rushwa, utakatishaji fedha na ukwepaji kodi kwenye ofisi zao zilizoko nje kidogo ya jiji la Paris.

Kiongozi huyu mwenye umri wa miaka 63 mpaka sasa amekataa kujibu wito wa kuhojiwa katika kesi hiyo, kesi ambayo imekuwa ikimuandamana tangu amalize muhula wake mwaka 2012.

Kuzuiliwa kwa Sarkozy kuliripotiwa kwa mara ya kwanza na gazeti linaloandika habari za uchunguzi la Le Monde.

Mtoa taarifa ambaye yuko karibu na jopo la uchunguzi amethibitisha kuwa hata Brice Hortefeux aliyekuwa waziri kwenye serikali ya Sarkozy pia alihojiwa siku ya Jumanne kama sehemu ya uchunguzi.

Kiongozi huyu alikuwa kiini cha uchunguzi uliofunguliwa mwaka 2013 na majaji ambao awali walidai kuwa Gaddafi na mtoto wake Seif al-Islam walitoa fedha kusaidia kampeni ya Sarkozy.

Sarkozy mwenyewe ameendelea kukanusha tuhuma kuwa alikuwa na uhusiano wa karibu na uliokuwa utawala wa Libya na baadae kushiriki katika kuivamia nchi hiyo na kuumaliza utawala wa miaka 41 wa Gaddafi.

Mfanyabiashara raia wa Ufaransa mwenye asili ya Lebanon Ziad Takieddine amesema alifanya safari tatu kutoka Tripoli na Paris katika mwaka wa 2006 na 2007 akiwa na fedha taslimu kwaajili ya kusaidia kampeni ya Sarkozy.

Taarifa zinasema kuwa kila mara alipokuwa akibeba fedha zilikuwa ni kati ya euro milioni 1 hadi 2, amesema Takieddine alipohojiwa na kituo cha televisheni cha Ufaransa na kuongeza fedha hizo alipewa na mkuu wa idara ya ujasusi wa Libya Abdallah Senussi.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.