Shirika la ndege la Afrika Kusini lamuomba radhi mwanariadha mwenye ulemavu
Shirika la ndege nchini Afrika Kusini “SAA” limemuimba radhi mwanariadha mwenye ulemavu na mshindi wa medali ya fedha Tyrone Pillay, baada ya kukatazwa kuingia kwenye ndege yake na miguu ya bandia.
Imechapishwa:
Tukio hili lilitokea Jumanne ya wiki hii, wakati mwanariadha huyo akirejea nyumbani akitokea kushiriki michezo ya Olimpiko ya Rio, Brazil kwa watu wenye ulemavu, ambapo alishinda medali ya fedha.
Mwanamichezo huyo aliweka wazi malalamiko yake kwenye ukurasa wa Twitter, akidai kuwa wafanyakazi wa shirika la ndege la Afrika Kusini, SAA, walimzuia kuunganisha ndege kutoka jijini Johannesburg kwenda Durban, nyumbani kwake ambapo alikuwa amebeba miguu ya bandia ambayo ni ya akiba.
Mwanamichezo huyo aliandika kuwa “huduma mbaya zaidi kwa mwanamichezo mwenye ulemavu, wakati wafanyakazi wa ndege walipokataa nisibebe miguu yangu.” ilisema twitter yake.
“Siamini kama naweza kuhudumiwa hivi baada ya kuishindia nchi yangu medali, ni jambo la kusikitisha kabisa,” alisema mwanamichezo huyo.
Mwanamichezo huyo aliruhusiwa kubeba miguu ya bandia na shirika hilo hilo la ndege akitokea Sao Paulo hadi Johannesburg.
Shirika la ndege la Afrika Kusini ndio lilikuwa shirika lililopewa mamlaka ya kuwasafirisha wanamichezo wa nchi hiyo walioenda kushiriki michezo ya Olimpiki nchini Brazil.
Msemaji wa shirika hilo Tlali Tlali amesema kuwa, shirika lao limeomba radhi kwa Pillay, kutokana na tukio ambalo hata wao hawakulifurahia.
Shirika hilo limesema linachunguza tukio hilo. Pillay alizaliwa akiwa na upungufu kwenye miguu yake na alihitaji kifaa maalumu kutembelea.