Kiongozi mwingine wa Kamati ya Olimpiki nchini Kenya akamatwa
Polisi nchini Kenya wameendelea kuwakamata wakuu wa Kamati ya taifa ya Olimpiki kutokana na tuhma za wizi na matumizi mabaya ya Ofisi zinazowakabili baada ya kumalizika kwa Michezo ya Olimpiki nchini Brazil mwezi huu.
Imechapishwa:
Hatua hii inakuja baada ya wanamichezo wa nchi hiyo hasa wanariadha kulalamika kuwa hawakupata huduma nzuri ikiwemo makaazi na hata makocha wengine kukosa vibali wakati wa Michezo hiyo.
Aidha, inadaiwa kuwa wanamichezo walipata sare moja tu badala ya nne huku maafisa wa Kamati hiyo wakiambatana na wapendwa wao katika Michezo hiyo kinyume na utaratibu.
Madai haya yameikasirisha serikali ya Kenya na kutaka viongozi wote wa NOCK kuchunguzwa ili kubaini ukweli kuhusu madai haya.
Fridah Shiroya Mwekahazina wa Kamati hiyo ndio afisa wa juu wa hivi karibuni kukamatwa na polisi na kuhojiwa kuhusu madai hayo.
Siku ya Jumanne, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Kipchoge Keino naye pia alihojiwa na kuachiliwa huru.
Tayari Katibu Mkuu wa Kamati hiyo Francis Paul na aliyekuwa Meneja wa kikosi cha Kenya Pius Ochieng, wameshatakiwa na kuachiliwa kwa dhamana ya Shilingi za Kenya 200,000 kila mmoja.
Waziri wa Michezo nchini humo Hassan Wario tayari amevunja Kamati hiyo ya Michezo ya Olimpiki.