Rais wa zamani wa Shirikisho la riadha nchini Kenya afariki dunia
Aliyekuwa rais wa Shirikisho la riadha nchini Kenya AK Isaiah Kiplagat amefariki dunia.
Imechapishwa:
Kiplagat aliyeongoza Shirikisho hilo kwa muda wa miaka 23 amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 72 baada ya kusumbuliwa na ugonjwa wa saratani kwa muda mrefu.
Mbali na kuongoza Shirikisho hilo, Kiplagat alihudumu pia katika nyadhifa mbalimbali ikiwemo kuwa Makamu wa rais wa Shirikisho hilo na kuwa Katibu Mkuu.
Mwaka 2015, aliachia urais wa Shirikisho hilo ili awanie Umakamu rais wa Shirikisho la riadha duniani IAAF lakini akapoteza.
Mwezi Novemba mwaka huo baada ya Uchaguzi wa IAAF, alipigwa marufuku kushiriki katika maswala ya riadha kwa; madai ya kutotoa ushirikiano katika suala la madai ya wanariadha kutumia dawa za kusisimua misuli lakini pia kutumia visivyo ufadhili kutoka kampuni ya Nike.
Hata hivyo, wakati akiwa hai, alikuwa anakanusha madai hayo.