Donald Trump : Mimi si mbaguzi wala sijafikiria kufanya hivyo
Rais wa Marekani Donald Trump amesema yeye si mbaguzi, baada ya kauli yake wiki iliyopita kuhusu wakimbizi kutoka barani Afrika na Haiti.
Imechapishwa:
Trump alinukuliwa akiyafananisha mataifa ya Afrika kama shimo la kutupa taka, wakati akihoji ni kwanini wahamiaji waliendelea kuja Marekani.
Trump ameeleza kuwa, hajawahi kuwa mbaguzi na kusisitiza kuwa, hajawahi kufikiria kufanya hivyo.
Rais huyo wa Marekani amekuwa, akipata shinikizo kuomba radhi mataifa ya Afrika baada ya kutoa matamshi hayo ya kudhalilisha Waafrika.
Tangu alipoingia madarakani mwaka uliyopita, Trump amekuwa akionesha wazi kuwa hataki tena wahamiaji kuendelea kuja Marekani na tayari amewazuia wahamiaji kutoka mataifa sita ya kiislamu kuingia nchini humo.
Tume ya Umoja wa Mataifa ya Haki za binadamu, pia ililaani matamshi hayo na kuyaita kuwa ni ya kichochezi.