Tunisia: Wahamiaji 13 wa Sudan wafariki katika ajali ya meli, 27 hawajulikani walipo
Wahamiaji 13 wa Sudan wamefariki na ishirini na saba hawajulikani walipo baada ya boti yao ya chuma kuzama siku ya Alhamisi kutoka pwani ya Tunisia karibu na Sfax, Farid Ben Jha, msemaji wa mahakama ya Monastir, ameliambia shirika la habari la AFP.
Imechapishwa:
Jumla ya Wasudan 42 walikuwa kwenye boti hiyo iliyoondoka pwani ya Jebiniana, karibu na Sfax (katikati-mashariki), kulingana na ushuhuda uliyotolewa kwa mamlaka na manusura wawili pekee wa ajali ya boti hiyo. Operesheni inaendelea kujaribu kutafuta watu wengine waliotoweka katika ajali hiyo, amebainisha Bw. Ben Jha.
Wanaume na raia wote wa Sudan, waathiriwa walikuwa na kadi za waomba hifadhi zilizotolewa na Tume ya Juu ya Wakimbizi nchini Tunisia. Wakimbizi hawa walikuwa wamepanda boti ya chuma iliyo dhaifu sana, iliyotengenezwa kwa vipande vya chuma chakavu vilivyounganishwa kwa haraka, kulingana na habari ya shuhuda za kwanza zilizokusanywa.
Uchunguzi umefunguliwa ili kubaini majukumu, ameongeza Bw. Ben Jha, bila kuondoa uwezekano kwamba wahamiaji hao "walitumiwa katika kesi ya ulanguzi wa binadamu au katika kuunda kundi la uhalifu ili kujiunga na Ulaya kwa siri".
Tunisia pamoja na Libya,ni vituo vikuu vyaa kuondoka kwa maelfu ya wahamiaji wanaotaka kufika Ulaya kinyume cha sheria. Pwani za kwanza za Italia, pamoja na kisiwa cha Lampedusa, ziko chini ya kilomita 150 kutoka mkoa wa Sfax.
Katika kipindi cha miezi kumi na moja ya kwanza ya 2023, idadi ya wahamiaji haramu walionaswa na mamlaka ya Tunisia ilifikia watu 69,963, zaidi ya mara mbili ya uvamizi katika kipindi kama hicho cha mwaka uliopita, kulingana na takwimu zilizotumwa kwa shirika la habari la AFP na kuwasilishwa kwa msemaji wa sjeshi la Walinzi wa Taifa.
Kulingana na Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM), zaidi ya watu 2,270 walikufa mnamo mwaka 2023 katikati mwa Bahari ya Mediterania walipokuwa wakijaribu kufika Ulaya kisiri, au 60% zaidi ya mwaka uliopita.