Rais wa zamani wa Afrika Kusini awataka wabunge wa ANC kuweka mbele maslahi ya wananchi
Rais wa zamani wa Afrika Kusini Thabo Mbeki amewataka wabunge wa chama tawala cha ANC kufanya maamuzi kwa kuzingatia maslahi ya wananchi wala sio chama hicho.
Imechapishwa:
Mbeki ametoa kauli hii kuelekea mjadala muhimu bungeni wa kukosa imani na rais Jacob Zuma wiki ijayo.
Wanasiasa wa upinzani wamesema wamechukua hatua ya kuwasilisha mswada huo bungeni baada ya rais Zuma kumfuta kazi Waziri wake wa fedha Pravin Gordhan wiki mbili zilizopita, uamuzi ambao ulikashifiwa sana nchini humo.
Inadaiwa kuwa ras Zuma alimfuta kazi Waziri huyo kutokana na juhudi zake za kupambana na ufisadi ndani ya serikali.
Hata hivyo rais Zuma kwa upande wake amesema alichukua hatua hiyo kwa madai kuwa Waziri huyo alikuwa mfisadi.
Wabunge wa chama cha ANC wamegawanyika kuhusu hili huku maandamano makubwa yakishuhudiwa wiki iliyopita kumshinikiza Zuma kuachia ngazi.
Kamati kuu ya chama hicho kinasema hakijaona sababu ya kumshinikiza rais Zuma ajiuzulu.
Muungano wa vyama vya wafanyikazi COSATU umemtaka Zuma pia kujiuzulu.