Pata taarifa kuu
BURUNDI-MAANDAMANO-USALAMA-SIASA

Waandamanaji waapa kutoondoka mitaani

Baada ya Baraza la Usalama la kitaifa nchini Burundi kutoa muda wa masaa 48 kwa waandamanaji wawe wamesitisha maandamnao na kuondoa vizuizi barabarani, viongozi wa mashirika ya kiraia na vyama vya upinzani walioandaa maandamano hayo, wamepuuzia onyo hilo.

Mmoja kati ya waandamanaji akishikilia bango dhidi ya muhula wa tatu wa Rais Nkurunziza, Bujumbura Mei 6.
Mmoja kati ya waandamanaji akishikilia bango dhidi ya muhula wa tatu wa Rais Nkurunziza, Bujumbura Mei 6. AFP PHOTO / PHIL MOORE
Matangazo ya kibiashara

Waandamanaji wameapa kutoodoka mitaani hadi pale Rais Pierre Nkurunziza ataachana na mpango wake wa kuwania muhula wa tatu katika uchaguzi ujao wa urais uliopangwa kufanyika Juni 26 mwaka 2015.

Kiongozi wa muungano wa vyama vya kiraia FOCODE, Pacifique Nininahazwe, amewatolea wito raia kuingia kwa wingi mitaani Jumapili asubuhi Mei 10, ili kuendelea kupinga muhula wa tatu wa Rais Nkurunziza.

Jumamosi mwishoni mwa juma hili, hali utulivu imeshuhudiwa katika mji mkuu wa Burundi, Bujumbura na katika baadhi ya mikoa, baada ya mashirika ya kiraia na vyama vya upinzani kutangaza Ijumaa wiki hii kusitishwa maandamano kwa siku ya jumamosi.

Wakati huo huo, baadhi ya wagombea kutoka vyama vya upinzani wamewasilisha faili zao za kugombea kwenye Tume huru ya uchaguzi Ceni. Wagombea hao ni pamoja na Agathon Rwasa, kiongozi wa kihistoria wa kundi la zamanai la waasi la Palipehutu-Fnl, Rais wa zamani Domitien Ndayizeye, pamoja na Jacques Bigirimana kiongozi wa chama cha Fnl.

Hata hivyo wagombea hao wamebaini kwamba hata kama wamewasilisha faili zao kwenye Tume huru ya uchaguzi Ceni, haimaanishi kuwa watashindana katika kinyanga'nyiro hicho na Rais Pierre Nkurunziza anaye maliza muda wake, wakisema kwamba Katiba ya Burundi pamoja na Mkataba wa amani na maridhiano wa Arusha havimruhusu kuwania muhula wa tatu.

Nchini Kenya, zaidi ya raia 250 waishio katika mji mkuu wa nchi hiyo, Nairobi, wameandamana mbele ya ubalozi wa Burundi, wakipinga muhula wa tatu wa Rais Nkurunziza. Waandamanaji hao wamemuomba Rais Nkurunziza kuachana na mpango wake wa kuwania muhula wa tatu katika uchaguzi ujao wa urais, wakibaini kwamba ni kukiuka Katiba ya Burundi na Mkataba wa amani na maridhiano wa Arusha.

Tume huru ya uchaguzi Ceni imetangaza kuwa kampeni za uchaguzi wa madiwani na wabunge zitaanza Jumapili Mei 10 na kumalizika Jumamosi Mei 23. Uchaguzi wa madiwani na wabunge umepangwa kufanyika Mei 24 mwaka 2015.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.