Ghala la tume ya uchaguzi lateketea kwa moto Kinshasa
Moja ya ghala kubwa za tume ya uchaguzi (CENI) katika mji mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Kinshasa, limeteketea kwa moto, vyanzo rasmi kadhaa vimelithibitishia shirika la habari la AFP, mjini Kinshasa.
Imechapishwa:
Moto huo uliozuka katika ghala hilo usiku wa Jumatano kuamkia Alhamisi wiki hii umesababisha hasara kubwa. Vifaa viliokuwa katika ghala hilo karibu vyote vimeteketea kwa moto.
Tukio hilo linatokea ikiwa zimesalia siku kumi kabla ya Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika Desemba 23.
"Moto ulizuka karibu saa nane usiku saa za Kinshasa (sawa na saa saba saa za Afrika ya Kati) katika moja ya ghala kuu ambapo kulikuwa kumehifadhiwa vifaa vya uchaguzi katika mji wa Kinshasa," amesema mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (CENI), Corneille Nangaa.
Wingu kubwa la moshi mweusi lilikuwa bado linaonekana saa mapema alfajiri, kwa mujibu wa televisheni ya shirika la habari la AFP.
Vifaa vya uchaguzi vilivyokuwa vimehifadhiwa katika ghala hilo ni pamoja na "mashine za kupigia kura" ambazo upinzani unapinga kutumiwa katika uchaguzi wa Desemba 23, ukidai kuwa zimepangwa kutumiwa kwa kuiba kura.
Le Président de la #CENI @CNangaa, accompagné des membres du bureau et de la plénière, s’est rendu aux entrepôts incendiés pour s’enquérir de la situation pic.twitter.com/1JdLQNwEd2
Ceni-rdc (@cenirdc) December 13, 2018
"Tunafanya tathmini kamili kuona jinsi gani ya kuendelea na uchaguzi wa Desemba 23 licha ya tukio hili," ameongeza mwenyekiti wa CENI.
Chanzo cha moto huo hakijafahamika bado, lakini uchunguzi unaendelea, kwa mujibu wa polisi mjini Kinshasa.