Kadinali Mosengwo alaani matumizi ya nguvu ya polisi dhidi ya waandamanaji DRC
Kadinali mwenye ushawishi mkubwa jijini Kinshasa Laurent Monsengwo Pasinya ameyaita matumizi ya nguvu ya polisi dhidi ya waumini wa kanisa katoliki walioandamana jumapili iliopita kuwa ni ya kishenzi wakati mkanganyiko kuhusu idadi ya watu walipoteza maisha ukiendelea kushuhudiwa.
Imechapishwa:
Kadianli Mosengwo amesema wanalaani na kutuhumu kwa msisitizo mwenendo wa watu ambao walitakiwa kuwalinda raia badala yake wanatekeleza kitendo cha kishenzi dhidi ya watu ambao walitakiwa kupewa ulinzi.
Upande wake baraza la maaskofu wa kanisa katoliki nchini DR Congo limesema halijagawanyika kama inavyotangazwa na baadhiya watu na kwamba wanaungana kwa pamoja kulaani vurugu za polisi kanisani dhidi ya waumini wa kanisa katoliki.
Hayo yanajiri wakati huu waandaji wa maandamano wakieleza kwamba watu 12 ndio walipoteza maisha huku polisi ikieleza kwamba hakuna mtu aliefia kanisani na kwamba watu zaidi ya 60 waliotiwa nguvuni waliachiwa huru. Waziri wa haki za binadamu nchini DR Congo Marie Ange Mushobekwa amesema Polisi haijatumia nguvu zaidi kama inavyoelezwa.
Wakati huo huo vuguvugu linalodai mageuzi nchini DR Congo Lucha, linasema wanachama wake 40 walitiwa nguvuni, huku 16 wakiachiwa huru, wengine wakiendelea kuzuiliwa katika mazingira magumu.
Taarifa zaidi kutoka jijini Kinshasa zinaeleza kuwa ripota maalum wa RFI jijini Kinshasa Florent Maurice alizuiliwa kwa dakika kadhaa wakati alipokuwa akiandaa ripoti katika chumba cha kuhifadhia maiti katika hospitali Mama Yemo kuhusiana na taarifa ya kuzuiliwa kwa familia za waathirika wa vurugu za Jumapili.