Upinzani watoa wito wa kuendelea kwa maandamano
Mji wa Kinshasa ulishuhudia Jumanne Januari 20 siku ya pili ya makabiliano kati ya polisi na vijana wanaompinga rais Kabila, ambaye upinzani unamtuhumu kujaribu kufanya mbinu za kusalia madarakani kupitia sheria mpya ya uchaguzi, ambayo inaleta utata nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Serikali imetangaza jana Jumannne kwamba machafuko yaliyodumu siku mbili tangu Jumatatu Januari 19, yamegharimu maisha ya watu 5, lakini upande wa mashirika ya kiraia wamebaini kwamba idadi ya watu waliouawa katika machafuko hayo inaweza kuwa juu zaidi.
Wakati huo huo kiongozi wa kihistoria wa upinzani dhdi ya kabila, Etienne Tshisekedi, akiwa mjini Brussels, nchini Ubelgiji, ametolea wito upinzani na raia wazalendo wa Congo kuutimua utawala wa kiimla ambao unamkandamiza mwananchi.
Nae Kardinali Monsengwo kupitia tangazo alilotoa, amelaani mpango wa marekebisho ya sheria ya uchaguzi nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Hali ya utulivu iliripotiwa jana Jumanne jioni katika mji wa Kinshasa, huku kukionekana idadi kubwa ya askari polisi katika mitaa mbalimbali ya mji huo, kwenye maeneo muhimu hususan majengo ya serikali, kama vile majego ya Baraza la Seneti.
Mjadala kuhusu sheria ya uchaguzi, unatazamiwa kuanza tena kabla ya Alhamisi wiki hii katika majengo ya Baraza la Seneti. Hata hivyo upinzani umewatolea wito wafuasi wake kumiminika barbarani ili kupinga mpango huo wa kujaribu kuifanyia marekebisho sheria ya uchaguzi.
Hayo yakijiri upinzani umetoa wito wa kuachiliwa kwa Jean-Claude Myambo, kiongozi wa SCOD, moja ya vyama vya upinzani. Jean-Claude Myambo alikamatwa Jumanne Januari 20 asubuhi.