Mataifa 6 ya Afrika yatatuma ujumbe wa amani kwa Urusi na Ukraine
Nairobi – Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa ,amesema kuwa viongozi sita wa Afrika wanapanga kusafiri hadi Urusi na Ukraine katika juhudi za kusaidia kupata suluhu la vita hivyo.
Imechapishwa:
Mapema leo , Ramaphosa amesema kuwa Rais wa Urusi Vladimir Putin na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky wamekubali kupokea ujumbe huo na wakuu wa nchi za Afrika, huko Moscow na Kyiv.
Ramaphosa alisema alifanya mazungumzo kwa njia ya simu na viongozi hao wawili ambapo aliwasilisha mpango ulioandaliwa na Zambia, Senegal, Jamhuri ya Kongo, Uganda, Misri na Afrika Kusini.
"Nilikubaliana na Rais Putin na Rais Zelensky kuanza na maandalizi ya mazungumzo na wakuu wa nchi za Afrika," Ramaphosa alisema.
"Tunatumai tutakuwa na majadiliano ya kina," alisema, akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari huko Cape Town wakati wa ziara ya serikali ya Waziri Mkuu wa Singapore Lee Hsien Loong.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres na Umoja wa Afrika (AU) wamefahamishwa kuhusu mpango huo na kuukaribisha,
Ramaphosa hakutoa ratiba maalum ya ziara hiyo au maelezo mengine, akisema tu kwamba mzozo umekuwa "wa kuangamiza" na Afrika "pia inateseka sana" kutokana nayo.
Nchi za Afrika zimeathiriwa vibaya na kupanda kwa bei ya nafaka na athari kwa biashara ya dunia.
Tangazo hilo limekuja siku moja baada ya Ramaphosa kusema Afrika Kusini imekuwa chini ya "shinikizo la ajabu" kuchagua upande katika mzozo huo, kufuatia shutuma kutoka kwa Marekani kwamba Pretoria ilisambaza silaha kwa Moscow hatua ambayo ingevunjwa na madai yake ya kutoegemea upande wowote.
Misheni hiyo itakuwa ya hivi punde katika msururu wa juhudi za kidiplomasia ambazo hazijafanikiwa hadi sasa kumaliza vita.