Syria: Uwanja wa ndege wa Damascus haufanyi kazi tena baada ya mashambulizi ya Israel
Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Damascus umelengwa na mashambulizi ya anga ya Israel ambayo yamesababisha uwanja huo kufungwa Jumapili hii mchana, Novemba 26, kulingana na shirika linalotetea haki za binadamu la Syria na vyombo vya habari vya serikali. Uwanja wa ndege wa mji mkuu wa Syria ulishambuliwa mara mbili tangu kuanza kwa vita huko Gaza Oktoba 7.
Imechapishwa:
Na mwandishi wetu wa kikanda, Paul Khalifeh
Uwanja wa ndege wa Damascus ulifungwai saa 24 baada ya kuanza tena shughuli zake. Uwanja huo wa ndege ulikuwa halutumiki tangu Oktoba 22 baada ya mashambulizi ya Israel ambayo yalisababisha uharibifu mkubwa wa miundombinu yake.
Shirika linalotetea haki za binadamu la Syria limeripoti kuwa makombora ya Israel yaligonga njia za ndege kwenye uwanja huo wa ndege siku ya Jumapili.
Mamlaka ya Syria imetangaza kwa upande wake kwamba makombora yaliyorushwa na ndege za Israel kutoka Milima ya Golan inayokaliwa kwa mabavu na Israel yaliangushwa na mfumo wa Ulinzi wa anga wa Syria. Makombora mengine, hata hivyo, yaligonga maeneo kadhaa katika uwanja wa ndege na katika maeneo mengine ya Damascus, vyanzo vya Syria vimeongeza bila kutoa maelezo zaidi.
Shirika linalotetea haki za binadamu linaripoti kwa upande wake kwamba mlipuko mkubwa ulisikika katika eneo la uwanja wa ndege wa kijeshi wa Mazze, karibu na mji mkuu.
Mamlaka ya Damascus imetangaza kwamba safari zote za ndege zimeelekezwa kwenye viwanja vya ndege vya Aleppo na Latakia kaskazini.
Israel inasema viwanja vya ndege vya Syria vinatumiwa na Iran kupeleka vifaa vya kijeshi kwa Hezbollah ya Lebanon.
Waangalizi wa haki za binadamu, hata hivyo, wamesema wakati wa shambulio la Oktoba 22, kwamba hakuna shehena ya silaha au risasi iliyotua katika viwanja vya ndege vya Syria tangu kuanza kwa vita vya Gaza, Oktoba 7.