Uturuki inafikiria kujiunga na kesi ya mauaji ya halaiki ya Afrika Kusini dhidi ya Israel
Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki Hakan Fidan ametangaza kuwa Uturuki imeamua kujiunga na kesi ya Afrika Kusini dhidi ya Israel ya mauaji ya halaiki huko Gaza katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki.
Imechapishwa:
"Uturuki imeamua kuungana na Afrika Kusini katika kesi ya mauaji ya halaiki dhidi ya Israel katika mahakama ya ICJ," Hakan Fidan alisema katika mkutano wa pamoja na waandishi wa habari mjini Ankara na mwenzake wa Indonesia, Retno Marchudi, uliofanyika mwishoni mwa mazungumzo baina ya nchi hizo mbili ambayo yalilenga kuhusu hali ya Gaza. .
"Tunatumai kwamba hatua hii itasaidia kuelekeza mchakato katika ICJ katika mwelekeo sahihi," amebaini, akiongeza kuwa juhudi za Uturuki kujiunga na kesi hiyo zimekuwa zikiendelea kwa "muda mrefu".
Amesema hivi karibuni Ankara itakamilisha kazi yake ya kisheria kuhusu suala hilo.
Fidan amesisitiza tena kuwa Uturuki itaendelea kuwaunga mkono watu wa Palestina "katika hali zote", na kufanya kazi na nchi zote rafiki na washirika ili kuamua hatua zaidi zinazowezekana na kutambua nchi zinazoweza kujiunga na ombi hili.
Mwezi Desemba, Afrika Kusini iliwasilisha malalamiko dhidi ya Israel katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki, ikiishutumu kwa kufanya mauaji ya halaiki huko Gaza. Uamuzi wa muda wa mwezi Januari uliiamuru Tel Aviv kukomesha vitendo vya mauaji ya halaiki na kuchukua hatua zinazohitajika kuhakikisha msaada wa kibinadamu kwa raia wa Gaza.
Vita visivyokoma vya Israel dhidi ya Gaza tangu tarehe 7 Oktoba vimesababisha karibu watu 35,000 kupoteza maisha, wengi wao wakiwa wanawake na watoto, na maelfu zaidi kujeruhiwa na kusababisha uharibifu mkubwa na uhaba mkubwa wa mahitaji ya kimsingi.
Israel pia imeweka mzingiro mkali kwenye eneo la pwani, na kuwaacha wengi wa wakazi wake, hasa wakaazi wa kaskazini mwa Gaza, kwenye ukingo wa njaa na kukosa maji safi na dawa. Zaidi ya miezi sita baada ya kuanza kwa vita vya Israeli, sehemu kubwa ya Gaza iko katika magofu, na kusukuma 85% ya wakazi wa eneo hilo kutoroka mashambulio ya mara kwa mara, kulingana na Umoja wa Mataifa.