HRW yalaani Israel kutumia nguvu kupita kiasi dhidi ya watoto wa Kipalestina
Jeshi la Israel na polisi wa mpakani wanaua watoto wa Kipalestina katika hali ambayo uwajibikaji haupo kabisa. Haya yamebainishwa na uchunguzi wa shirika la kimataifa la Haki za binadamu la Human Rights Watch uliochapishwa Jumatatu asubuhi. Shirika la kutetea haki za binadamu linashutumu matumizi yasiyo ya uwiano, ya kimfumo na haramu ya kikos cha mauaji dhidi ya Wapalestina, hasa watoto.
Imechapishwa:
Mnamo Novemba 21, 2022, Mahmoud al-Sadi, Mpalestina mwenye umri wa miaka 17, akiwa njiani kuelekea shuleni katika kambi ya wakimbizi ya Jenin, majeshi ya Israel yalifanya uvamizi katika eneo hilo. Urushianaji risasi na wapiganaji wa Kipalestina yaliripotiwa. Kijana huyo alisubiri kando ya barabara makabiliano hayo yamalizike. Akiwa hana silaha, hana kifaa chochote kinachoweza kumdhuru mtu, aliuawa kwa risasi zilizofyatuliwa kutoka kwa gari la kijeshi.
Kesi hii bado inafuatiliwa, anasema Éric Goldstein, naibu mkurugenzi wa Human Rights Watch kwa Mashariki ya Kati: “Tuko mwezi Agosti na tangu mwanzoni mwa mwaka huu, watoto 34 wa Kipalestina katika Ukingo wa Magharibi wameuawa kwa risasi za Israel. Sasa tuko katika kiwango kibaya zaidi kwa miaka kumi na tano, tangu karibu Intifada ya 2 ( harakati za mapambano) ianze. "
'Ukiukaji wa wazi wa sheria za kimataifa'
Watoto hawa hawakutoa vitisho vya moja kwa moja. Ni "ukiukaji wa wazi wa sheria ya kimataifa", inabainisha ripoti ya HRW. Na matumizi ya nguvu kupita kiasi, yaliyofanywa bila kuadhibiwa kabisa, anaendelea Éric Goldstein: “Hakuna uchunguzi unaofunguliwa moja kwa moja kunapotokea uhalifu huo."
Katika kukabiliana na ukatili huu wa kutisha, ripoti inasema, washirika wa Israel wanapaswa kutoa shinikizo kuwawajibisha wale waliohusika na unyanyasaji huu...na kukomesha tabia hiyo.